WAZIRI Mkuu Edward Lowassa amewaonya na kwamba hatakuwa na simile wala huruma kwa wafanyakazi wazembe na wasiotimiza wajibu wao ipasavyo.
Lowassa alitoa onyo hilo jana wakati akizungumza na wafanyakazi wa ofisi yake mjini Dar es Salaam mara baada ya kuingia kwa mara ya kwanza tangu ateuliwe kushika wadhifa huo wiki iliyopita.
Taarifa iliyotolewa na Mwandishi wa Habari wa Waziri Mkuu, Jacob Tesha ilimkariri Lowassa akisema kuwa Serikali ya awamu ya nne ingependa kuona wafanyakazi na wananchi kwa jumla wakibadilika na kufanya kazi kwa bidii.
Alisema kuwa, wananchi wana matumaini makubwa na awamu hii ya serikali na hivyo yeye kama Waziri Mkuu asingependa kuona wafanyakazi wakiendelea kufanya kazi kwa mtindo aliouita kuwa wa ‘mazoea’.
Badala yake alisisitiza kuwa ni lazima utendaji kazi nchini sasa uendane na ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya.
“Wananchi wetu wana mategemeo makubwa kutoka kwa serikali ya awamu na nne. Itabidi tubadilike… tufanye kazi kwa bidii,” alisema.
“Haiwezekani wafanyakazi wakaendelea kufanya mambo vilevile kama walivyozoea. Sitakuwa na simile katika hili,” alionya.
Lowassa ambaye ni mbunge wa Monduli aliapishwa mjini Dodoma Ijumaa iliyopita na Rais Jakaya Kikwete kuwa Waziri Mkuu wa Serikali ya awamu ya nne baada ya kuthibitishwa na Bunge kwa kura 312 kati ya 314 zilizopigwa.
Waziri Mkuu Lowassa anachukua nafasi ya Waziri Mkuu mstaafu Frederick Sumaye aliyekuwa Waziri Mkuu kwa kipindi cha miaka kumi mfululizo kuanzia l995 katika serikali iliyoongozwa na Rais mstaafu Benjamin Mkapa.