Na Dennis Msacky
HAKIKA Jakaya Kikwete ambaye ni mgombea urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), ni miongoni mwa wanasiasa ambao wana mvuto mkubwa kwa jamii. Mvuto huu na mengine mengi ndio uliomwezesha kuweza kuibuka mshindi katika mchakato mgumu wenye ushindani mkali wa kumpata mgombea urais katika chama chake.
Haiba ya Kikwete ni wanasiasa wachache sana wenye nayo. Wengi huvuma katika kipindi kifupi na baada ya hapo wanasahaulika. Wapo wanasiasa kama marehemu Oscar Kambona, Austine Lyatonga Mrema waliovuma kwa kishindo katika siasa za Tanzania, lakini kadri siku zilivyokwenda, mvuto wao kwa jamii ulishuka.
kwa Jakaya Kikwete hilo, halipo kwani kwa miaka zaidi ya kumi amekuwa kipenzi cha wanaCCM walio wengi na hata kwa Watanzania pia. Moja ya sifa aliyonayo Kikwete ni ile ya kuwa karibu na watu. Kushiriki katika shughuli za kijamii, nazo zimemfanya mgombea huyu awe kipenzi cha watu na hasa wajumbe wa chama hicho.
Kikwete ni mwanasiasa asiyejiona hata pale ambako angetarajiwa kujiengua na kujiweka kwenye ngazi za ukubwa, ni mtu tofauti na wanasiasa wengine wa taifa hili.
Wengi walidhani mara baada ya kupelekwa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa tangu mwaka 1995-2005, basi umaarufu wake katika siasa za ndani ya nchi ungepungua, lakini haikuwa hivyo. Nafasi hii iliweza kumpa upeo mkubwa kuhusu masuala ya nje.
Alizidi kupanda chati, ndio maana aliweza kuwaangusha vigogo wengine waliokuwa wanawania nafasi hiyo ndani ya chama. Aliibuka na ushindi mkubwa, ulioacha washindani wake hoi.
Kupanda chati katika medani ya kisiasa kwa Kikwete pia kutokana na uwezo wake kiakili wa kujifunza mambo.Kwanza hakuna ubishi kwamba Kikwete amekomaa katika siasa, kwani alianzia katika uwanja wa Vijana akishika nyadhifa za siasa na utendaji. Kote huku aliweza kumudu vema.
Pia ni miongoni mwa mawaziri katika serikali ya sasa, waliofanya kazi katika wizara nyingi. Amefanya kazi katika wizara tatu, Nishati (Maji) na madini, Fedha na sasa mambo ya nje, pia kwa kipindi kirefu amekuwa katika Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM na baadaye Kamati Kuu ya Chama, Ana utumishi wa miaka 30 ndani ya CCM.
Kutokana na Kung'aa kwa nyota ya Kikwete kisiasa, anapewa nafasi kubwa ya kupotea kijiti kutoka kwa Rais Benjamin Mkapa, ambaye anamaliza muda wake baada ya kutumikia nchi kwa vipindi viwili vya miaka mitano mitano kwa mujibu wa katiba ya nchi.
Mkapa anamaliza kipindi chake cha miaka10 hapo Oktoba baada ya Uchaguzi Mkuu. Ushindi wa Kikwete unaonekana dhahiri kutokana naye kuwa mpenzi mkubwa wa wananchi wengi, na pia chama anagombea kupitia chama kilichodumu katika uongozi wa nchi kwa zaidi ya miaka 40. Hivyo kina mikakati imara ya kuweza kunyakua ushindi.
Hata katika mchakato mzima wa kumpata mgombea wa CCM, hakika haikuwa kazi rahisi kwani aliweza kupambana na vigogo waliokuwa wakionekana kwamba wanakubalika pia katika chama, kama vile aliyekuwa Katibu Mkuu wa iliyokuwa Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU), Dk. Salim Ahmed Salim, waziri wa mawasiliano na uchukuzi, Pro. Mark Mwandosya. Pamoja na wagombea wengine wanane walioshika ngazi mbalimbali.
Kikwete, alizaliwa mwaka 1950, na ana shahada ya kwanza katika uchumi aliyoipata katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Katika miaka hiyo ya 1970, Kikwete angeweza kujiendeleza zaidi katika fani ya uchumi, lakini kutokana na mapenzi yake katika siasa na kuipenda TANU, aliamua kujikita zadi katika ajira ya chama, ambayo kwa madai yake ilikuwa haina kipato kizuri.
Hata hivyo, baadaye alijiunga na Jesho la Wananchi wa Watanzania (JWTZ), alikopata nyadhifa kadhaa ikiwamo ya kuwa mkuu wa masuala ya usalama katika jeshi hilo.
Hata baada ya kuingia jeshini, alirudi katika siasa na hatimaye akaingia bungeni miaka ya 80, Nyota yake iliendelea kung'ara na Mzee Ali Hassan Mwinyi alimwona akampa wadhifa za Unaibu waziri kisha waziri kamili.
Alikuwa miongoni mwa mawaziri wachache wa serikali ya awamu ya pili waliorejeshwa katika awamu ya tatu, akikabidhiwa mikopo ya Mambo ya Nje tangu mwaka 1995 hadi sasa.
Harakati zake za kutaka kuukwaa urais wa Tanzania zilianza mwaka 1995, alipoangushwa na Rais Benjamin Mkapa katika mchakato wa kupata mgombea urais kupitia CCM. Hata hivyo, isingekuwa ni utaratibu wa ushindi wa theluthi mbili, Rais wa awamu ya tatu angekuwa ni Kikwete, Kwani katika raundi ya kwanza wakati wa kura ndani ya Mkutano Mkuu wa CCM mwaka 1995, aliongoza, mbele ya Rais Mkapa wa Waziri Mkuu wa zamani, Cleopa Msuya. Ilikuwa ni raundi ya pili iliyompambanisha Kikwete na Rais Mkapa ndiyo iliyompa ushindi Rais Mkapa.
Uhodari wake na umakini wake, hata baada ya kushindwa mwaka 1995, ulimweka Kikwete kwenye mstari safi. Aliweza kumpongeza Mkapa pale pale Chimwaga na kutangaza kuvunja kundi lake na kulitakalijiunge na Mkapa kumpungia kampeni dhidi ya wagombea wa vyama vingine.
Watu wengi wanamwona Kikwete kwamba ni mtu asiyejiona na ambaye amekulia katika misingi ya Baba wa Taifa, Julius Nyerere. Hii ni kutokana naye kutojilimbikiza mali. Pia amekuwa mtu wa karibu na jamii na hii ndio iliyomfanya azidi kupendwa.
Tayari amekwisha kutangaza kauli miu yake: "Ari mpya, Nguvu mpya na Kasi Mpya," amekwisha kutambua kazi kubwa iliyoko mbele yake, sasa anajipanga kuitekeleza.
Katika uchaguzi wa mwaka huu, atakuwa anapambana na mgombea wa CUF, Prof. Ibrahim Lipumba ambaye anaonekana kukua kisiasa kadri siku zinavyokwenda.
Pia atakuwa na anapambana na mgombea mwingine kutoka CHADEMA, Freeman Mbowe ambaye anaonekana kuwa mvuto katika sehemu anazopita kukijenga chama chake.
kama Kikwete ataukwaa urais atakuwa na kazi moja kubwa nayo ni kuendeleza yale ambayo Mkapa ameonyesha katika uongozi wake. Mkapa ameweza kufufua uchumi wa Tanzania, ambao ulikuwa umedidimia na kuleta heshima ndani na nje ya nchi.
Gazeti-Mwananchi
ISSN-0856-75724 Tarehe Jumapili 21 Agosti 2005