Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete, amewataka wapiga kura wa majimbo mawili ya Rungwe kuwachagua Profesa David Mwakyusa wa Jimbo la Mashariki na Profesa Mark Mwandosya wa Rungwe Magharibi kwa sababu anawahitaji katika utumishi.
Bila kufafanua anataka kuwatumia kwa njia gani, Mhe. Kikwete aliwasihi wapiga kura kuwachagua wagombea hao kwa sababu anawajua, ni waadilifu na wanaweza kumsaidia katika utendaji wake wa kazi.Hata hivyo, Profesa Mwandosya alipita bila kupingwa katika jimbo lake.
Akihutubia maelfu ya watu katika Kiwanja cha Michezo mjini Tukuyu, mgombea huyo alimsifia Dr. Mwakyusa kwa kusema kuwa alijitahidi sana kuokoa maisha ya mwasisi wa Tanzania, marehemu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Hata hivyo haikuwezekana. Profesa Mwakyusa alikuwa daktari wa Mwalimu.
"Nilipokwenda kumtembelea Mwalimu kule St. Thomas Hospital, nilimkuta Dr. nakumuuliza kama inawezekana kuokoa maisha yake. Dr. Mwakyusa aliniambia kuwa 'mimi kama daktari nimemaliza. Kilichobaki ni cha Mungu. Nilimuuliza alikuwa na maana gani? Akaniambia kuwa nilivyosema ndivyo ninavyomaanisha," alisema Kikwete. Kuhusu Profesa Mwandosya, Kikwete alisema anamfahamu kwa sababu walifanya wote kazi katika Wizara moja na kisha katika serikali moja.
katika mkutano huo, Kikwete aliwatahadhalisha wananchi wa Wilaya ya Rungwe juu ya tatizo la ukimwi na kusema kuwa maambukizi katika wilaya hiyo sasa yamefikia kiwango cha asilimia 22.5
"Pamoja na kwamba serikali itaongeza kasi ya kuwapatia dawa za kupunguza makali ya ukimwi, njia nyepesi na ya uhakika ni kuwa na tahadhali katika tabia zetu," alisema mgombea huyo.