Mke wa Rais Mama Salma Kikwete amesema uteuzi wa Dkt Asha- Rose Migiro na Balozi Liberata Mulamula kushika nyadhifa za juu katika nyanja za kidiplomasia, kuwe changamoto kwa wanawake wengine hapa nchini kufanya vema katika shughuli zao mbalimbali.
Ameyasema hayo leo jioni wakati alipokuwa akisalimiana na wake wa Mabalozi na Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa hapa nchini. Mama Kikwete alikuwa ameandaa hafla fupi kwa lengo la kusalimiana, kufahamina, kubadilisha mawazo na uzoefu kuhusu mambo muhimu yanayohusu maendeleo ya wanawake na watoto.
“Mwaka 2006 ulikuwa mwaka muhimu kwa wanawake wa Tanzania, kwangu mimi binafsi na kwa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA). Katika mwaka huo tulishuhudia wanawake wakingia katika anga za diplomasia za kimataifa. Mafanikio ya wanawake hawa ni chachu kwa wanawake wengine” alisema Mama Kikwete.
Mama Salma Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo,(WAMA) alisema uteuzi wa Migiro kuwa Naibu Katibu Mkuu wa UN na Mulamula kuwa KatibuMtendaji wa Sekretariet ya Nchi za Maziwa Makuu kumpa shauku na hamasa ya kutaka kuwaona wanawake wengi zaidi wakifikia hatua za juu zaidi.
Aidha alisema ndio maana ameamua kuwasaidia na kuwaendelea watoto wa kike ili nao waweze kuja kushika nyadhia za juu katika taasisi mbalimbali ndani na nje ya nchi.
Akielezea mikakati yake ya kuwasaidia watoto wa kike kupata elimu ya juu, Mama Kikwete alisema hadi sasa wanafunzi wa kike 140, kutoka Tanzania Bara na Visiwani, wamepata ufadhili wa WAMA wa kuendelea na masomo ya sekondari katika shule za Umma na za Binafsi.
Alisema ili kufanikisha juhudi za kumwendeleza mtoto wa kike kielimu na kuwapatia maisha bora wanawake, ushirikiano wa karibu unahitajika kati ya taasisi yake na wake za mabalozi hao kupitia chama chao pamoja na wadau wengine.
Pamoja na kuelezea mikakati ya kumwendeleza mtoto wa kike kielimu, Mama Kikwete alisema taasisi yake pia imejikita katika vita dhidi ya ukimwi mkazo ukiwa kwa vijana na mapambano dhidi ya ugonjwa wa malaria.
Katika hafla hiyo, Mama Salma Kikwete aliusifu mchango wa Mama Anna Mkapa kupitia taasisi yake ya Mfuko wa Fursa Sawa kwa Wote (EOTF) kwa namna alivyochangia kusukuma mbele maendeleo ya wanawake na watoto hapa nchini.
Alisema kuwa kazi kubwa na nzuri iliyofanywa na Mama Mkapa, ndiyo iliyomsukuma na yeye kuendeleza kazi hiyo ya kuwasadia wanawake na watoto wa Tanzania kwa kuanzisha WAMA ili wapate maisha bora.
Akizungumza kwa niaba ya wake za mabalozi hao, Mke wa Balozi wa Sweden, alimshukuru Mama Salma Kikwete kwa kuwakutanisha pamoja na wakampongeza kwa jitihada anazofanya za kuwaendeleza wanawake na watoto hapa nchini.
Wake hao wa mabalozi wameahidi kumpa ushirikiano wa hali na mali ili aweze kutekeleza majukumu aliyojipangia.