Hotuba Ya Rais Kwenye Kilele Cha Sikukuu Ya Mei Mosi 2007
Guestbook
Tanzania, is a country on the east coast of east Africa.
 
JakayaKikwete.com
 »  Home  »  Habari Mpya  »  Hotuba Ya Rais Kwenye Kilele Cha Sikukuu Ya Mei Mosi 2007
Hotuba Ya Rais Kwenye Kilele Cha Sikukuu Ya Mei Mosi 2007
By Ikulu Press | Published  05/1/2007 | Habari Mpya , Speeches | Rating:
HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE, KWENYE KILELE CHA SIKUKUU YA WAFANYAKAZI DUNIANI, MWANZA, MEI MOSI 2007

 

 

Ndugu Rais  wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Nchini (TUCTA),

    Ndugu Johari Juma;

Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana,

    Mheshimiwa John Chiligati;

Waziri wa Kazi, Maendeleo ya Vijana, Wanawake na Watoto wa

    Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,

    Mheshimiwa Asha Abdallah Juma;

Waheshimiwa Mawaziri na Wabunge;

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza;

Mheshimiwa Getruda Mongela, Rais wa Bunge la Afrika;

Mama Maria Ducci, Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu ILO;

Mama Regina Njaku ¨C Mkurugenzi wa ILO Kanda ya Afrika;

Mwakilishi wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) Kanda ya Afrika Mashairiki,

      Mheshimiwa Jurgen Schwettmann;

Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Waajiri (ATE),

    Dkt. Aggrey Mlimuka;

Waheshimiwa Mabalozi:  Balozi wa Cuba na Balozi wa Uganda ;

Wawakilishi wa Vyama vya Siasa na Serikali;

Ndugu Wafanyakazi na wananchi Wenzangu;

Mabibi na Mabwana:

Ndugu Wafanyakazi;

          Naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, kwa kutujalia uhai na afya njema mambo ambayo yametuwezesha kukutana leo katika sherehe za mwaka huu za Siku ya Wafanyakazi Duniani tunazoziadhimisha hapa jijini Mwanza.  Ni wajibu kushukuru, kwani kuna baadhi ya wenzetu kwa sababu ya matatizo ya kiafya wanashindwa kujumuika nasi.

       Kadhalika wako wenzetu hawapo nasi kwa sababu wametangulia mbele za haki.  Miongoni mwa wenzetu hao ni Ndugu yetu mpendwa Faustin Musita aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa aliyetutoka tarehe 24 Aprili, 2007.

          Napenda kutumia nafasi hii kuwapeni pole wananchi wenzetu wa Mwanza na wafanyakazi wote nchini kwa msiba mkubwa huu uliotupata sote. Kifo cha Musita ambaye pia alikuwa Mratibu wa sherehe hizi za Mei Mosi

hapa Mwanza ni pigo kubwa siyo tu kwa jumuia ya wafanyakazi nchini, bali pia kwa taifa letu kwa jumla.

          Mimi binafsi nilimfahamu marehemu kwa kipindi kirefu. Alikuwa mjumbe mwenzangu wa Kamati ya Utekelezaji ya kwanza ya Umoja wa Vijana wa CCM (1978 ¨C 1984). Ndugu Musita alikuwa mchapa kazi hodari na mzalendo wa hali ya juu.  Alikuwa mtu muwazi na msema kweli asiyeogopa, hivyo sikushangaa alipochaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa.  Marehemu alitumia muda wake mwingi hapa duniani kuwahudumia na kuwatumikia wanadamu wenziwe kwa moyo na nguvu zake.

      Aidha, alikuwa kiongozi shupavu wa wafanyakazi aliyetetea maslahi yao kwa ujasiri na bila kuchoka. Ni dhahiri kifo chake kimeacha pengo kubwa siyo tu kwa familia yake, bali pia kwa nchi yetu kwa ujumla. Tunamwomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi. Amin.

       Nawashukuru sana Viongozi wa Vyama Huru vya Wafanyakazi Tanzania kwa heshima hii kubwa mliyonipa ya kuwa Mgeni Rasmi kwenye sherehe hizi kwa mara ya pili mfululizo.

          Nawashukuruni pia viongozi na wananchi wa mkoa wa Mwanza kwa mapokezi yenu mazuri na makubwa yaliyojaa upendo tele.  Mimi siwashangai kwani wenyeji wa mkoa huu mnayo sifa kubwa ya ukarimu na upendo kwa wageni.  Tunachokishuhudia leo ndiyo ukweli wa sifa yenu hiyo. 

          Napenda niwapongeze pia viongozi na wananchi wa mkoa huu chini ya uongozi wa Mkuu wa Mkoa, Mheshimiwa James Msekela, kwa kazi kubwa na nzuri mliyoifanya ya kuandaa sherehe hizi.  Natambua uzito na ugumu wa mzigo mliobebesywa lakini kwa ushirikiano mzuri baina yenu na wawakilishi wa wafanyakazi pamoja na Wizara ya Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana sherehe hizi zimefana kiasi hiki.  Kwa niaba ya wageni wenzangu nawashukuru, nasema hongereni sana.

          Niruhusuni pia niwapongezeni kwa dhati wafanyakazi wenzetu hodari waliotangazwa na kuzawadiwa hapa leo.

      Tuzo mlizopata leo ni uthibitisho wa utendaji kazi wenu mzuri. Naomba hii iwe ni chachu na motisha ya kuwafanya muongeze bidii zaidi kazini ili mwakani muendelee kuwa wafanyakazi bora. Nchi yetu itajengwa na wafanyakazi kama ninyi mnajituma na  kufanya kazi kwa ufanisi na nidhamu kazini. Ni matumaini yangu kuwa ushindi waliopata wenzetu hawa  utakuwa kichocheo kwa wafanyakazi wengine kuongeza bidii kazini ili mwakani na nao wawe washindi na kupokea tuzo.

 

Maslahi ya Wafanyakazi

Ndugu Wafanyakazi;

          Baada ya shukrani na pongezi hizo, sasa naomba mniruhusu niwaeleze hatua tuliyofikia katika kutekeleza baadhi ya ahadi nilizozitoa kwenu mwaka wa jana kwenye mkutano na viongozi wa Wafanyakazi na hotuba yangu kujibu risala yenu.  Nianze na uboreshaji wa mishahara na maslahi ya watumishi wa umma.

          Mtakumbuka kuwa katika hotuba yangu ya Shinyanga nilisema kuwa serikali inatambua kilio cha watumishi wa umma kuhusu mishahara na maslahi yao kwa ujumla. Niliwaahidi mambo mawili katika kushughulikia tatizo hili.  Kwanza , niliwaahidi kuwa licha ya nchi na uchumi wetu kukabiliwa na matatizo kadhaa, bado watumishi wa umma watapata nyongeza ya mishahara katika mwaka wa fedha 2006/2007.  Pili kwamba, nitaunda Tume ya kutoa mapendekezo kuhusu namna ya kuboresha maslahi ya wafanyakazi wa umma nchini.

          Napenda kuwaarifu kuwa tumetimiza ahadi yetu kwa mambo yote mawili. Katika mwaka huu wa fedha yaani 2006/2007 tumeongeza mishahara ya watumishi wa umma kwa asilimia 5 hadi 15. Tarehe 12 Mei, mwaka wa jana wiki mbili tu baada ya kauli yangu pale Shinyanga, niliunda Tume ya Kuboresha Maslahi ya Watumishi wa Umma. 

Tume ya Kuboresha Maslahi ya Watumishi wa Umma

          Tume hiyo iliyokuwa chini ya Ndugu yetu Deogratius Ntukamazina, ilikuwa na jukumu la kupendekeza juu ya namna bora ya kuboresha maslahi ya watumishi nchini.  Ilitakiwa kupendekeza  misingi, uwiano na taratibu katika kufanya marekebisho ya mishahara ya watumishi wa umma ikiwa ni pamoja na mchakato mzima wa kuelekea kwenye kulipa mishahara inayotosheleza mahitaji ya maisha (living wage).  Kadhalika ilikuwa na jukumu la kuangalia juu ya masuala mengine yahusuyo maslahi ya wafanyakazi kama vile pensheni na mengineyo.

          Tume ya Ntukamazina ilianza kazi rasmi tarehe 01 Julai, 2006.  Na kama ambavyo wengi wenu mnafahamu Tume hiyo tayari imekamilisha kazi yake na kunikabidhi rasmi taarifa yake tarehe 22 Januari mwaka huu.  

          Napenda kuitumia nafasi hii kwa mara nyingine tena kutoa pongezi za dhati kwa wajumbe wa Tume ya Ntukamazina kwa kazi nzuri waliyoifanya.  Wamefanya uchambuzi wa kina ulio yakinifu kuhusu hali ilivyo kwa upande wa maslahi ya watumishi wa umma hapa nchini.  Tume pia imetoa mapendekezo muafaka ya namna ya kushughulikia suala zima la kuboresha maslahi ya wafanyakazi wa umma nchini.

          Serikali kwa upande wake imekuwa inayachambua

na kuyafanyia kazi mapendekezo mbali mbali ya Tume

// hiyo. 

 hiyo.  Dhamira yetu ni  kutekeleza mapendekezo ya Tume hiyo, hatua kwa hatua, kadri uwezo unavyoruhusu.  Katika mwaka ujao wa fedha yaani 2007/2008 tutaanza mchakato wa utekelezaji na kuendelea nao miaka ijayo. 

          Hivyo nawasihi watumishi wa umma kuwa na subira na wazidi kufanya kazi kwa kujituma zaidi ili kukuza uchumi na hivyo kuongeza mapato ya Serikali.  Kukua kwa uchumi na kuongezeka kwa mapato ya Serikali ndiko kutakakoongeza uwezo wa Serikali kuboresha maslahi ya watumishi wa umma mapema zaidi.

          Tukumbuke kuwa nyama nyingi na maziwa mengi siku zote hupatikana kwa ng¨®mbe aliyenona kwa kupata matunzo na malisho mazuri.  Hivyo hivyo, ikiwa tutafanya bidii katika kukuza uchumi, serikali itapata mapato zaidi kupitia kodi.  Serikali ikipata mapato zaidi ndipo itakapoweza kuboresha maslahi ya wafanyakazi wake na kutimiza vizuri zaidi wajibu wake kwa taifa na wananchi wake.

      Kwa sababu hiyo, naomba kukumbusha wajibu wetu sote, viongozi, wafanyakazi, wakulima, wawekezaji na wananchi kwa ujumla wa kufanya kazi kwa bidii zaidi na maarifa katika kukuza na kuendeleza uchumi wetu.

          Maisha bora ya Mtanzania yataletwa na kukua kwa uchumi. Na kukua kwa uchumi kutaletwa na sisi wenyewe kwa kufanya kazi kwa bidii na maarifa; kila mmoja wetu mahali pake pa shughuli aifanyayo.

 

Bodi za Mishahara ya Kima cha Chini

NduguWafanyakazi;

          Jambo la tatu nililoahidi, linalohusiana na maslahi ya wafanyakazi katika sekta binafsi. Nilizungumzia uharakishaji wa uundaji wa Bodi za Kisekta za Kima cha Chini cha Mishahara.  Nilielezea kutokuridhishwa kwangu na hali ilivyokuwa mwaka wa  jana na nikaiagiza Wizara ya Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana kuongeza kasi ya uundwaji wa Bodi hizo.

          Nafurahi kwamba tangu wakati huo kasi ya kuunda Bodi hizo imeongezeka na hali inaleta matumaini.  Tayari Bodi zimeundwa katika sekta nane yaani:-

 

¡ö       Sekta ya Huduma za Majumbani

¡ö       Sekta ya Huduma ya Biashara na Viwanda

¡ö       Sekta ya Madini

¡ö       Sekta ya Huduma za Afya

¡ö       Sekta ya Huduma za Majini, Bahari na Maziwa

¡ö       Sekta ya Huduma ya Ulinzi Binafsi

¡ö       Sekta ya Kilimo

¡ö       Sekta ya Usafiri na Huduma za Usafirishaji.

 

     Nafurahi pia kuwa kazi ya kutengeneza kanuni imekamilika na siku chache zijazo zitazinduliwa.

     Mchakato wa kuunda Bodi kwenye sekta nyingine unaendelea kwa wadau, ambao ni pamoja na waajiri na wafanyakazi, kutoa mapendekezo yao serikalini.Ni matumaini yangu kuwa zoezi hilo litaharakishwa ili uundaji wa Bodi katika sekta zilizobakia ufanyike mapema iwezekanavyo.

            

              

      

      

Ndugu Wafanyakazi;

        Bodi hizi ni muhimu sana katika mfumo wetu wa sasa wa kushughulikia maslahi ya wafanyakazi nchini.  Uamuzi wa mishahara na maslahi ya watumishi wa umma hufanywa na Serikali.  Zamani serikali ilikuwa inaamua hivyo kwa wafanyakazi wote nchini hata wale wa sekta binafsi.  Siku hizi, utaratibu umebadilika.  Maamuzi ya kima cha chini cha mishahara kwa wafanyakazi wa sekta binafsi hufanywa na Bodi za Kisekta.  Serikali inalo jukumu la kuhakikisha kuwa bodi hizo zinaundwa na kuteua wajumbe wake.

        Nafurahi kusema kuwa wajumbe wa zile Bodi  nane zilizokwishaundwa wameshateuliwa na kuanza kazi. Ombi langu kwa wajumbe wa Bodi hizo ni kwamba wajitahidi kutekeleza majukumu yao kwa ukamilifu mapema iwezekanavyo. Kilio cha maslahi duni kwa watumishi wa sekta binafsi ni cha kweli, tena ni cha muda mrefu.  Sasa fursa ya kuyashughulikia matatizo yao imepatikana, naomba itumike vizuri mapema iwezekanavyo. 

 

     Ni ukweli ulio wazi kuwa wafanyakazi katika sekta binafsi wanalipwa mishahara duni na maslahi yasiyoridhisha hata kidogo.  Kwa kawaida, kote duniani wafanyakazi wa sekta binafsi wanalipwa vizuri zaidi kuliko wenzao wa sekta ya umma. Mwelekeo siku zote huwa wafanyakazi wa umma kukimbilia sekta binafsi. Hapa kwetu ni kinyume chake.

        Ni jambo la kusikitisha kuona kwamba baadhi ya waajiri kwenye sekta binafsi wanawalipa wafanyakazi wao ujira mdogo sana ambao kwa kweli unawadhalilisha. Mazingira ya kazi nayo si mazuri hata kidogo mambo ambayo yanahitaji kurekebishwa.

     Ni matumaini yangu kuwa Bodi za Kima cha Chini za Kisekta zitasaidia katika kutafuta ufumbuzi na matatizo hayo kutoka sekta binafsi.  Aidha, ni matarajio yangu kuwa Bodi hizo zitapata ushirikiano kutoka kwa waajiri na wafanyakazi.   

        Waajiri wanao wajibu wa kujali maslahi ya wafanyakazi wao pamoja na kujali lengo lao la kupata

 faida. Kupata faida kwa kuwapunja mishahara wafanyakazi wao si sawa. Kwa kweli si jambo halali hata kidogo.  Nawaomba wajali maslahi ya wafanyakazi wao ili kuboresha mahusiano baina yao . Naamini wakifanya hivyo mahusiano yao yatakuwa mazuri.

         

Suala la Ajira

Ndugu Wafanyakazi;

          Suala la kukuza ajira tumelipa kipaumbele cha juu katika agenda ya Serikali yetu.  Ni moja ya ahadi kuu za CCM kwa Watanzania zilizotajwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama chetu.  Nilielezea mkakati wetu wa kukuza ajira serikalini na katika sekta binafsi.  Kadhalika nilielezea dhamira yetu ya kuanzisha utaratibu wa kuwasaidia watu kujiajiri.

            Katika hili, kubwa tulilolifanya ni kuanzisha mpango wa mikopo ya wajasiriamali wa shilingi bilioni 21 kwa Tanzania Bara yaani bilioni moja kwa kila mkoa. Kiasi hicho kimeongezwa maradufu kutokana na maelewano yetu na

mabenki. Mpango huu unawalenga hasa wanyonge kwa kuwapatia mikopo yenye masharti nafuu.  Kama tulivyokwishafafanua shabaha yetu  ni kwamba watu waitumie mikopo hiyo kuanzishia shughuli za uzalishaji mali na huduma zitakazowaongezea kipato na hivyo kuinua hali zao za maisha na kupunguza umaskini.

          Tulianza kutekeleza mpango huu mwezi Januari 2007 na hadi sasa mwitikio wa wananchi umekuwa wa kuridhisha sana .  Watu wengi binafsi, vikundi vingi na SACCOS nyingi zimejitokeza kuomba mikopo hiyo kiasi kwamba maombi yamezidi fedha iliyotengwa kwa lengo hilo .  Hii ni dalili nzuri inayoonyesha dhahiri jinsi gani Watanzania tulivyo na kiu ya kujiletea maendeleo na kuondokana na umaskini.

          Serikali itaendelea kuwasiliana na vyombo husika ikiwa ni pamoja na benki za NMB na CRDB ili kuhakikisha kuwa mpango huu unafanikiwa na unawanufaisha wananchi wanyonge walio wengi wakiwemo wafanyakazi wa hali ya chini.

 

          Vile vile tutaendelea kujenga mazingira mazuri ya uwekezaji ili kuwavutia wawekezaji wengi zaidi wa ndani na nje.  Tutaendeleza zoezi tulilokwisha lianza la kuondoa vikwazo vya kuanzisha na kufanya biashara nchini ili wawekezaji wengi zaidi wa ndani na nje ya nchi yegtu wavutike na kuja kuwekeza hapa nchini.

      Kufanya hivyo kutakuza ajira na kupunguza kilio cha watu wengi na hasa vijana. Muelekeo ni mzuri tunachotakiwa kufanya ni kusimamia na kutekeleza kwa ukamilifu na kwa dhati maamuzi yetu hayo.  Sisi Serikalini tunafanya hivyo, nawaomba wadau wengine nao watimize ipasavyo wajibu wao kwa maslahi yetu sote.

Ajira ya Wageni

          Kuhusu tatizo la wageni kuajiriwa katika nafasi za kazi ambazo zingeweza kufanywa na Watanzania, ninachoweza kuwaambia leo ni kuwa serikali imeendelea kuchukua hatua za kuziba mianya iliyokuwa inasababisha ulegevu katika kusimamia kanuni na taratibu zilizopo zinazohusu ajira ya wageni nchini.  Zoezi hilo ni endelevu.

Tutaendelea nalo hadi mambo yatakapokuwa yametengemaa.      

      Aidha, tutaendelea kuimairsha mafunzo ya kada ya kati hususani mafundi mchundo ambalo ndilo eneo kulikoshamiri zaidi ajira za wageni hivi sasa.  Nina hakika tukiyafanya haya tutaweza kuondokana na tatizo hili ambalo limekuwa likipigiwa kelele na watu wengi hapa nchini.

          Napenda kuwahakikishia wananchi kuwa serikali iko makini na itaendelea kuwa mtetezi imara wa maslahi ya watu wake likiwemo hili la ajira.  Tutazidi kusimamia kwa ukamilifu sheria zinazowalinda Watanzania dhidi ya wajanja wachache wanaotaka kutumia mwanya wa utandawazi kupindisha kanuni na taratibu tulizojiwekea.

 

Ushirikishwaji wa Wafanyakazi

Ndugu Wafanyakazi;

          Serikali inatambua umuhimu wa kuwapa wafanyakazi uhuru wa kutoa mawazo na kushiriki katika maamuzi mbalimbali yanayohusu uendeshaji wa taasisi wanazofanyia kazi.

Hii inatokana na ukweli kwamba kuna kutegemeana kati ya waajiri na waajiriwa, na kati ya Serikali, Waajiri na Vyama vya Wafanyakazi.  Kwa kutambua umuhimu huu serikali imeweka mazingira ya kisheria yanayowezesha utekelezaji  wa dhana hii.

          Hivyo, napenda kusisitiza rai yangu niliyoitoa mwaka wa jana kuwataka waajiri kuwashirikisha ipasavyo viongozi wa vyama vya wafanyakazi katika vikao mbalimbali vya utoaji maamuzi katika sehemu zao  za kazi. Nafurahi kwamba baadhi ya waajiri wametekeleza lakini wapo wengine bado. Narejea tena kauli yangu ya kuwataka wale ambao bado hawajatekeleza wafanye hivyo mapema iwezekanavyo. Nimemwagiza Waziri John Chiligati afuatilie jambo hili kwa karibu zaidi.

 

Ndugu Wafanyakazi;

          Mwaka wa jana mlitoa kilio chenu kuhusu mapungufu ya Mfuko wa Akiba ya Uzeeni wa Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa. Naliahidi kuchukua

hatua.  Nafurahi kuwaarifu kuwa tumetimiza ahadi yetu hiyo. Mfuko huo wa Akiba ya Wafanyakazi sasa ni Mfuko wa Pensheni wa Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa kama ilivyo kwa mifuko mingine. 

      Hii sasa inawahakikishia wafanyakazi wa Serikali za Mitaa mafao bora zaidi wanapofika mwisho wa utumishi wao. Napenda kuwahakikishia kuwa, tuko tayari kuchukua hatua zaidi na zipasazo kuboresha zaidi mfuko huo pale panapostahili.

 Malipo ya Mafao ya Wafanyakazi wa iliyokuwa EAC

Ndugu wafanyakazi na Watanzania Wenzangu;

          Katika kutambua na kuthamini haki za wafanyakazi na mchango wao mkubwa kwa nchi yetu, Serikali tangu Julai 2005, imekuwa ikitekeleza ahadi yake ya kuwalipa mafao wananchi waliokuwa wafanyakazi wa iliyokuwa Jumuia ya Afrika Mashariki iliyovunjwa mwaka 1977.  Zoezi la kuwalipa lilianzishwa na Serikali ya Awamu ya Tatu na sisi tunaliendeleza.

          Jumla ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya zoezi hili ni shilingi 117 bilioni. Kati ya fedha hizo serikali imekwishatumia shilingi bilioni 115 kuwalipa wastaafu 36,405 tokea zoezi lianze hadi kufikia tarehe 30 Machi, 2007.

          Malipo ya mirathi ya wastaafu waliokwishatangulia mbele ya haki yamekuwa yakifanyika kwa kupitia mahakama mbalimbali nchini.  Idadi ya mirathi yote iliyokwishalipwa hadi sasa ni 7,666 yenye thamani ya shilingi 30.9 bilioni.

          Aidha, kati ya malipo yote yaliyokwishafanyika hadi sasa wastaafu 6,888 bado hawajajitokeza  na jumla ya shilingi 22.9 bilioni bado hazijalipwa kwa sababu hiyo. Napenda kutumia nafasi hii kuwaomba wale wote wanaohusika kujitokeza kuchukua malipo hayo ambayo ni haki yao .

          Na kama katika orodha tutagundua kuwa watu hawajalipwa, tutatafuta fedha tuwalipe.

 

Mikataba ya Madini

Ndugu Wananchi;

          Jambo lingine ambalo nililizungumzia mwaka jana lilihusu mikataba ya madini.  Katika hotuba yangu ya Shinyanga nilizungumzia haja ya nchi yetu kutazama

upya mikataba hiyo ili tuweze kunufaika na rasilimali ya madini aliyotujaalia Mwenyezi Mungu.  Nilisema pamoja na kuthamini sana mchango wa Makampuni ya madini yaliyowekeza hapa nchini, bado kuna haja ya kuweka utaratibu mzuri utakaotuwezesha sisi wenye rasilimali nao tufaidike.

          Aidha, niliagiza Wizara ya  Nishati na Madini ishirikiane na Wizara ya Sheria na Katiba, Wizara ya Uchumi, Mipango na Uwezeshaji na Wizara ya Fedha na makampuni husika kuangalia upya Sheria yetu ya Madini na mikataba tuliyowekeana kwa lengo la kufanya marekebisho stahiki.

          Katika kutekeleza agizo hilo , Agosti 10, mwaka wa jana  Kamati Maalum ya majadiliano ya mikataba ya madini iliundwa.  Kamati hiyo ilikuwa na jukumu la kufanya mashauriano na Tanzania Chamber of Minerals and Energy (TCME) kuhusu mfumo wa kodi katika sekta ya madini.  Pia ilikuwa na jukumu la kufanya majadiliano na makampuni ya madini yenye mikataba ya madini na serikali kwa lengo la kurekebisha kasoro zilizopo.

 

Ndugu Wananchi;

          Nafurahi kuwafahamisha kuwa, majadiliano kati ya serikali na makampuni makubwa ya madini hapa nchini yamekuwa na mafanikio.  Tayari kampuni ya Barrick Gold Tanzania Limited na Resolute Mines Tanzania Limited  zimekubali kuondoa kipengele cha kivutio cha asilimia 15 kwenye salio la gharama ya uwekezaji katika migodi yao . Hatua hii itayafanya makampuni haya sasa kulipa kodi ya mapato  miaka michache ijayo tofauti na ilivyokuwa kabla ya hapo ambapo yasingelipa kodi kwa uhai mzima wa migodi yao .

          Mazungumzo yanaendelea na makampuni mengine kufanya kama ilivyokuwa kwa makampuni haya mawili. Muda si mrefu nchi yetu nayo itaanza kunufaika ipasavyo na utajiri mkubwa wa dhahabu tuliyojaaliwa na Mwenyezi Mungu.

          Kampuni ya Barrick Gold pia imekubali kuilipa serikali kiasi cha dola za Kimarekani milioni 7.0 kwa mwaka kwa kila mgodi inaoumiliki kuanzia mwezi

 

 

Desemba, 2006 hadi mwaka 2010.  Malipo hayo ni mbali na dola za Kimarekani 200,000 ambazo kampuni hiyo na ile ya Resolute itazilipa kila mwaka Halmashauri za wilaya ambako kuna migodi yake.

          Hivi sasa tunapitia Sera na Sheria yetu ya madini kwa lengo la kuzifanyia marekebisho stahiki katika muda si mrefu ujao.  Nia yetu ni kuwa na sheria ya madini itayohakikisha kuwa pande zote mbili zinanufaika sawia yaani  sisi wenye rasilimali ya madini na makampuni ya uwekezaji yenye fedha na teknolojia. Tunataka Sheria hiyo ituwezeshe kuwa na mazingira ambayo  Waingereza wanayaita ¡°win¨Cwin situation¡±, yaani wao wanapata  na sisi tunapata.

 

Hitimisho

Ndugu Wananchi;

          Nimeona leo nisema hayo. Lakini, niwaahidi kuwa yale yote mliyoyasema kwenye risala yenu tutayatafakari na kuyafanyia kazi kama tulivyofanyia kazi yale

mliyoyasema mwaka wa jana. Napenda kuona kuaminiana na kushirikiana kunakuweko na kunazidi kukua baina ya nguzo zetu za utatu yaani Serikali, Waajiri na Wafanyakazi.

      Naomba nimalize kwa kuwashukuru tena kwa dhati wafanyakazi wote nchini kwa juhudi kubwa mnazozifanya katika kuimarisha uchumi wa nchi yetu na kuhudumia watu wake.  Tunatambua, tunathamini na kuheshimu mchango wenu adhimu.  Ukiufananisha uchumi wetu  na mwili wa mwanadamu, nyinyi ni uti wa mgongo.  Bila ya nguvu zenu uchumi wetu hauwezi kusimama wala kuimarika.

          Hivyo, napenda kumalizia kwa kuwahakikishia kuwa daima dumu serikali itawajali, itaendelea  kuwahudumia waajiri na wafanyakazi ili kwa pamoja waweze kutoa mchango mkubwa zaidi katika kujenga uchumi ulio imara na taifa imara lenye neema tele.

 

Mungu Ibariki Afrika!

     Mungu Ibariki Tanzania !

      Asanteni kwa Kunisikiliza.

 
How would you rate the quality of this article?
1 2 3 4 5
Poor Excellent

Verification:
Enter the security code shown below:
img


Add comment
Comments
  • Comment #1 (Posted by Israel A Mwakagugu)
    Rating
    Mpango wa kuongeza mishahara ya wafanyakazi wa Sekta binafsi ni uthibitisho tosha kwamba SERIKALI INA DHAMIRA NJEMA KWA WANANCHI.Sasa uwekezaji wa WAGENI utaleta maana nzuri ya kukuza ajira sio vibarua,uchumi wa mtu mmoja mmoja utakua.Tuna matumaini utekelezaji wake utaharakishwa.Tume zilizoundwa zisitumie vikao kwa ajili ya kutunisha Mifuko.Wanainchi Hatutambua TAARIFA NZURI WANAZOZIANDIKA KWENYE VIKAO,tutatambua umuhimu wa tume hizo tutakapoona sekta binafsi inaongeza Mishahara.Mabadiliko hayo yataongeza IMANI KWA SERIKALI ILIYO MADARAKANI.
     
Submit Comment