WAZIRI MKUU Edward Lowassa kesho (Jumatatu, Septemba 3, 2007) anatarajiwa kuanza ziara ya siku nne katika mkoa wa Ruvuma ambako atakagua shughuli mbalimbali zikiwemo ukaguzi wa viwanda vya korosho, kahawa na ufunguzi wa shule za sekondari.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege na kupokea taarifa za mkoa na chama, atakwenda wilaya ya Tunduru ambako atafungua chuo cha uuguzi cha KIUMA na kusalimiana na wananchi.
Jumanne atakagua ukarabati wa kiwanda cha Ubanguaji Korosho na kuhutubia mkutano wa hadhara katika uwanja wa michezo wa Tunduru.
Kwa mujibu wa ratiba hiyo, akitoka Tunduru, Waziri Mkuu atakwenda wilaya ya Namtumbo ambako atafungua sekondari ya Msindo na kusalimiana na wananchi kabla ya kuweka jiwe la msingi katika hosteli ya St. Benedict Hanga. Mchana atawenda kijiji cha Naikesi kufanya mkutano wa hadhara.
Kutoka Namtumbo, Waziri Mkuu atakwenda wilaya ya Mbinga ambako atapokea taarifa ya wilaya katika misheni ya Lituhi na baadaye kuhutubia mkutano wa hadhara kabla ya kuelekea mji mdogo wa Liuli. Akiwa Liuli ataweka jiwe la msingi katika madarasa ya shule ya sekondari ya St. Pauls, atasalimiana na wananchi na baadaye kuelekea mji wa Mbamba-Bay.
Kwa mujibu wa ratiba hiyo, Waziri Mkuu atawasili Mbinga Mjini na kufungua kiwanda cha kukoboa kahawa na kuhutubia mkutano wa hadhara katika uwanja wa michezo wa mjini Mbinga na jioni hiyo hiyo anatarajiwa kurejea jijini Dar es Salaam.