Serikali ya Awamu ya Nne inaendelea kutekeleza ahadi zake iliyozitoa wakati wa
kampeni za Urais kama ilivyoainishwa na Ilani ya Chama Cha Mapinduzi.
“Tuliahidi kufanya jitihada za kuinua huduma bora za kiuchumi na kijamii
ili kuinua hali ya maisha ya Watanzania na kuongeza kipato cha mwananchi” Rais
Kikwete amewaambia wananchi wa Somanga wakati wa kukabidhi vifaa mbalimbali kwa
wananchi wa Somanga vitakavyowasaidia katika shughuli zao za uvuvi.
Jumla ya shilingi milioni 125 zimetengwa kwa ajili ya kuvisaidia vikundi
mbalimbali katika wilaya za Kilwa, Mafia na Rufiji.
Rais Kikwete pia ameweka jiwe la msingi katika kituo cha umeme wa gesi
asilia cha Somanga, ambacho ni moja ya kilio cha wananchi wa Kilwa wakati wa
kampeni.
Rais aliahidi huduma hiyo na sasa imeshafikia hatua ya awali ambapo huduma
ya umeme inatarajiwa kuanza mapema mwaka ujao.
“Tumetimiza ahadi, na tunasema tunatenda na tutatenda yote tuliyoahidi
wananchi zikiwemo huduma za afya, elimu, maji, umeme na kuongeza tija katika
shughuli mbalimbali za kilimo na kiuchumi” amesema.
Kituo cha Umeme cha Somanga kitanufaisha wananchi wapatao 3500 katika
vijiji mbalimbali wilayani Kilwa na mara kitakapokamilika kitakabidhiwa kwa
Shirika la Umeme la Tanzania (TANESCO) ili kukiendesha.
Katika huduma za jamii, Wilaya ya Kilwa imepiga hatua katika ujenzi wa
shule za sekondari kwa kutimiza lengo la kila kata kuwa na shule ya sekondari na
kupeleka watoto shule kwa asilimia 96.
Wilaya ya Kilwa pia inakabiliwa na uhaba wa maji salama kwa matumizi ya
binadamu na kufikia Julai 2007, Serikali ilishatenga shilingi milion 404.6 kwa
ajili ya kufanyia ukarabati mabomba na visima mbalimbali katika vijiji 58
wilayani humu.
Katika bajeti ya mwaka huu, Serikali pia imetenga shilingi bilioni 1.48
kwa ajili ya huduma mpya ya maji kwa vijiji 10 na inatarajiwa kuwa ifikapo
mwanzo wa mwaka ujao, visima vipatavyo vitano vitaanza kutoa huduma hiyo kwa
wananchi.
Rais Kikwete pia ameeleza azma ya Serikali kuhakikisha barabara ya
Kilwa-Mbwemkulu-Mingoyo kuwa kazi inaendelea vizuri na kukamilika mapema
iwezekanavyo na kwamba kipande kilichobaki cha Somanga-Darajani, chenye urefu wa
km, 60 kinafanyiwa utaratibu wa kupatiwa mkandarasi na kwamba matatizo yaliyopo
kwa sasa yatatatuliwa kama ilivyopangwa.
Rais Kikwete leo anaendelea na ziara wilayani Liwale ambapo anatarajiwa
kufungua daraja la Mto Ruhuhu.