Taarifa ya Ziara ya Rais Lindi - Nachingwea
Guestbook
Tanzania, is a country on the east coast of east Africa.
 
JakayaKikwete.com
 »  Home  »  Habari Mpya  »  Taarifa ya Ziara ya Rais Lindi - Nachingwea
Taarifa ya Ziara ya Rais Lindi - Nachingwea
By Premi Kibanga | Published  11/19/2007 | Habari Mpya | Unrated
 

Serikali inakamilisha taratibu za kuandika mradi wa maji kwa ajili ya Maji katika miji ya Masasi na Nachingwea na tayari mazungumzo ya kutafuta mfadhili kwa ajili ya mradi huo wa maji kutoka katika chemchemi ya Ndanda yameshaanza.


‘Nimeshawasilisha maombi ya mradi huo wa maji na mazungumzo yanaendelea kati ya Benki ya Maendeleo ya Uarabuni na Serikali, lakini pia Serikali inakamilisha taratibu za kuandika mradi huu ili fedha za wafadhili zikichelewa tuanze wenyewe” Rais Jakaya Kikwete amewaeleza wananchi wa Nachingwea katika mkutano wa hadhara leo mchana akiwa katika ziara mkoani Lindi..

Tayari Serikali inagharamia mradi mwingine mkubwa kwa ajili ya huduma za maji kwa wananchi wa Shinyanga na Rais Kikwete amesema amedhamiria kuleta huduma hii kwa wananchi kama alivyowaahidi katika kampeni za kutafuta kura mwaka 2005.

“Napenda kuwahakikishia wananchi wote kwamba tumeomba kazi ya utumishi na tumeianza, tunaendelea na tutaendelea nayo na kutimiza yale yote tuliyowaahidi wakati wa kutafuta kura” amesema.

Rais Kikwete amesema Serikali imedhamiria kuboaresha huduma za jamii kama vile elimu, afya, maji na miundo mbinu, pamoja na kuinua kipato cha wananchi ili maisha yao yawe bora zaidi kuliko vile yalivyokuwa kabla ya Serikali yake kushika uongozi wa Tanzania.

Akiwa mkoani Lindi kukagua shughuli za maendeleo na kuhakikisha kuwa ahadi zinatekelezwa kama alivyoahidi, Rais Kikwete amewaagiza viongozi akiwemo Naibu Waziri wa Miundo Mbinu Bw. Makongoro Mahanga, viongozi wa Wakala wa Barabara (TANROADS) na uongozi mzima wa mkoa wa Lindi kuhakikisha kuwa barabara zote mkoani humo, zinasimamiwa vilivyo ili zitengenezwe kufikia kiwango ambacho zitaweza kupitika katika kipindi chote..

Rais ametoa maagizo hayo baada ya mkandarasi aliyepewa kazi ya kutengeneza barabara mkoani humo kushindwa kuzikamilisha kwa muda na kiwango kinachotakiwa.

Rais amesema ni jambo la busara kama mkandarasi anashindwa kutimiza masharti akanyimwa kazi nyingine badala ya kupewa kazi sehemu ingine, wakati ameshadhihirisha kuharibu ile ya awali.

“Kama mkandarasi anashindwa kazi asipewe ingine ili wajifunze” Rais ameagiza.

Juhudi zingine za Serikali katika kutimiza ahadi kwa wananchi wa Nachingwea ni pamoja na kuunganishwa na miji ya Lindi na Mtwara katika kupata umeme kutokana na gesi ya Msimbati.

Serikali imeshatimiza baadhi ya ahadi katika wilaya za Mkoa wa Lindi ikiwa ni pamoja na ujenzi wa shule ambapo wilaya ya Nachingwea sasa inaandikisha watoto wenye umri wa kwenda shule kwa asilimia mia wilaya ina sekondari 14 na lengo la mwaka huu ni kuwa na sekondari 26 ambapo inatarajiwa kuwa ifikapo mwishoni mwa mwaka huu, shule zingine 12 zitafunguliwa.

Hata hivyo Mkoa wa Lindi pamoja na wilaya zake zinakabiliwa na tatizo kubwa la watoto kupata mimba na kujiingiza kwenye mapenzi hivyo kufanya idadi kubwa ya watoto kuacha shule kabla ya wakati.

Katika juhudi za Serikali kuinua maisha ya wananchi wake kwa ujumla, Serikali imesema inaliwekea mkazo swala la ununuzi wa Korosho ili bei isiyumbe na hatimaye kunufaisha wakulima.

Rais Kikwete amesema juhudi hizo ni pamoja na hatua ambayo Serikali imeshachukua ya kurithi madeni ya vyama vya ushirika ili vyama hivyo viweze kukopesheka na hatimaye bei ya korosho isiwe chini ya shilingi 610 kwa kilo ili mwaka huu wakulima wafaidike na hatimaye kuinua hali ya maisha yao.

Mara tu baada ya kuwasili wilayani Nachingwea, Rais amepokea taarifa ya utendaji ya wilaya ambapo pia amefungua nyumba za walimu wa shule ya msingi ya Mayaka, amefungua ghala la mazao katika kijiji cha Litula kabla ya kuongea na wananchi katika uwanja wa Sokoine.

Ghala la chakula la Litula ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa maendeleo wa Kilimo wa wilaya, shughuli ambayo inafanywa kupitia vikundi vidogo vidogo vya uzalishaji ambavyo viliwezeshwa na Mradi shirikishi wa maendeleo ya kilimo na uwezeshaji (PADEP).

Ghala hili litawanufaisha wakazi wapatao 1981 wa kijiji hicho ambao ni wakulima kwa kiasi kikubwa.

Rais anaendelea na ziara wilayani humo kesho.

How would you rate the quality of this article?
1 2 3 4 5
Poor Excellent

Verification:
Enter the security code shown below:
img


Add comment
Comments