Rais Jakaya Mrisho Kikwete leo amekagua barabara kuu ya Dar-Kibiti-Lindi hadi
Mingoyo na Masasi-Mangaka yenye urefu wa Km 480.8 pamoja na Daraja la Umoja
inayotarajiwa kukamilika mwezi ujao.
“Tuliwaahidi wakati wa kampeni kuwa mkituchagua barabara hii tutaikamilisha na
sasa imekamilika” Rais amewaambia wananchi katika sehemu mbalimbali akiwa njiani
kuelekea kutoka Lindi kwenda Kilwa kabla hajarejea Dar-es-Salaam baada ya
kukamilisha ziara yake mkoani Lindi. “Na tutaendelea kuwatumikia na hatimaye
kutimiza ahadi zote kama tulivyoahidi, nawahakikishia kazi tumeshaianza na
inaendelea vizuri,” Rais amesema.
Barabara hii imekuwa kero kwa wananchi wa mikoa ya kusini kwa miaka mingi tangu
1995 hadi kusababisha malalamiko toka kwa wananchi kuwa wamesahaulika, hivyo
kukamilika kwake kutaondoa adha na kuchochea maendeleo katika mikoa ya kusini
ambayo ina hazina kubwa katika kuleta maendeleo Tanzania.
Serikali imedhamiria kutumia pesa nyingi katika kutengeneza miundo mbinu na
huduma za kijamii kwa ujumla kama shule, hospitali na pia kuchangia katika
shughuli mbalimbali za kiuchumi za wananchi wake na kuboresha maisha yao
Ujenzi wa barabara hii uko kwa awamu ambapo hadi sasa Km. 129 za barabara kati
ya Dar-Kibiti zimekamilika kwa kiwango cha lami na Km. 4 zilizobaki zinatarajiwa
kukamilika mwezi ujao na kugharimu shilingi bilioni 15.
Barabara ya Ndundu-Somanga yenye urefu wa Km. 60 inatafutiwa mkandarasi ili
kuanza matengenezo chini ya udhamini wa Kuwait Fund, OPEC na Serikali ya
Tanzania.
Barabara ya Nangurukuru-Mbwemkuru yenye Km. 95 inatarajiwa kugharimu shilingi
bilioni 39.2 na inatarajiwa kukamilika mapema mwaka ujao. Km. zipatazo 78
zimekamilika kwa kiwango cha lami na ujenzi umefikia asilimia 93.
Barabara ya Mbwemkuru-Lindi-Mingoyo yenye urefu wa Km. 95 ina thamani ya
shilingi bilioni 51.5 nayo imeshakamilika kwa asilimia 94 kwa ikiwa ni Km. 84
kwa kiwango cha lami ambayo nayo itakamilika mwezi ujao.
Barabara ya Masasi-Mangaka yenye urefu wa Km. 54 itajengwa kwa awamu tatu ambapo
Km. 15 za lami zitagharimu shilingi bilioni 6.5 zitakapokamilika.
Rais pia amekagua Daraja la Umoja linalogharimiwa kwa ubia kati ya Tanzania na
Msumbiji ambapo tayari asilimia 58 ya ujenzi wake umekamilika na mradi mzima
utakamilika mwishoni mwa mwaka ujao.