HOTUBA
YA MGENI RASMI / MHESHIMIWA MAMA SALMA KIKWETE, MWENYEKITI WA WAMA WAKATI WA
KUFUNGUA MAONYESHO YA WASINDIKAJI YALIYOANDALIWA NA TAFOPA TAREHE 19 NOVEMBA
2007
Mlezi
wa TAFOPA – Mama Regina Lowassa
Mwenyekiti wa TAFOPA – Bibi SUZY LAIZER
Wageni waalikwa
Mabibi na Mabwana
Awali ya yote napenda kuchukua fursa hii kuwashukuru kwa kunipa heshima ya
kuwa mgeni rasmi katika kufungua maonyesho haya ya usindikaji vyakula. Pili
nawashukuru wanachama wa TAFOPA kwa kuandaa maonyesho haya muhimu.
Aidha naomba nitumie pia fursa hii kuwashukuru kwa dhati wafadhili
waliowawezesha kufanikisha maonyesho haya. Msaada huu ni muhimu sana kwa
wanachama wa TAFOPA kwa kuwa yanawapa fursa ya kujitangaza na sote
tunafahamu kuwa kujitangaza ni moja ya mbinu muhimu sana za kuleta mafanikio
katika Biashara.
Ndugu Mwenyekiti,
Uamuzi wa TAFOPA kuratibu na kufanya maonyesho haya ni jambo la kupongezwa
sana. Ni dhahiri kuwa uzoefu katika kuandaa maonyesho haya utawezesha
kuendelea kuandaliwa kwa maonyesho mengine ili kutoa fursa kwa wanachama na
wajasiriamali wengine kutangaza bidhaa zao, kujitafutia masoko na pia
kuwahamasisha watanzania kupenda bidhaa zinazozalishwa na watanzania ili
kuinua uchumi wa Taifa letu.
Ndugu zangu wana TAFOPA
Binafsi nimefurahishwa sana na juhudi zenu za kuandaa kitu kizuri kama hiki.
Hii ni changamoto kwa wajasiriamali wengine wadogo kujiunga na kutafuta
nguvu ya pamoja katika kupata masoko. Hili linawezekana.
Ndugu zangu, kuna kitu kimoja ningependa kukisema bayana. Katika ulimwengu
wa leo wa utandawazi kuna hatari ya wajasiriamali wadogo, kutupwa nje ya
ulingo wa biashara kwa sababu ya ushindani mkubwa wa kibiashara
unaowakabili.
Naamini wote mnatambua kuwa tunapozungumzia soko huria tunamaanisha haki na
fursa sawa za masoko. Mlaji anayo hiari ya kununua bidhaa aipendayo bila ya
kushurutishwa. Sasa ndugu zangu, nadhani kwa kuwa ninyi ni wafanayabiashara
mnaelewa ugumu uliopo katika kushindana kibiashara baina ya ninyi wachuuzi
wadogo na wazalishaji wakubwa wa viwandani.
Hii ni kwa sababu tofauti na wazalishaji wa viwandani, wajasiriamali wadogo
wengi wanakabiliwa na tatizo la ukosefu wa mitaji na teknolojia ya chini
wanayotumie hivyo kupunguza ubora wa bidhaa zao.
Hata hivyo ndugu zangu hilo lisiwakatishe tama. Kawa nilivyosema matatizo
haya yanazo suluhu. Mbinu ya kwanza ni kujiunga pamoja kama hivi mlivyofanya
ninyi, kwani sisi Waswahili tunasema “Umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu.”
Ndugu zangu wana TAFOPA,
Ni lazima mtafute ufumbuzi wa matatizo yenu kwa kuweka nguvu zenu pamoja.
Muwekeze akiba zenu ndani ya SACCOS yenu ili muweze kukopeshana. Imarisheni
umoja wenu mzidi kusonga mbele. Pia tengenezeni bidhaa bora zaidi ili muweze
kumudu soko la ushindani.
Mwenyekiti TAFOPA,
Serikali inatambua umuhimu wa wasindikaji wadogo katika kukuza uchumi, wa
Taifa, kutoa ajira na kuhifadhi mazao hasa wakati wa msimu wa mavuno. Kwa
kutambua hii, serikali imeandaa sera na mikakati mbalimbali ili kuhakikisha
kuwa inaweka mazingira mazuri, kuondoa leseni zisizokuwa za lazima ili
kuwasaidia wajasiriamali wadogowadogo.
Lakini kama nilivyosema, pamoja na sera hizi nzuri za serikali, mwamuzi wa
mwisho katika ununuzi wa bidhaa zako ni mlaji (mteja wako). Hivyo ni lazima
muhakikishe bidhaa mnazozalisha ni za ubora wa kiwango cha juu kabisa ili
kumvutia mlaji ili akila yeye asaidie kuwatangazia na wengine.
Ndugu zangu wana TAFOPA
TAASISI mbalimbali za fedha zimebuni mbinu za kuwasaidia wafanyabishara
wadogo muweze kupata mikopo. Aidha kuna MKURABITA na MKUKUTA ambazo
zinajenga mazingira ya kisheria ya kuwawezesha kuanzisha biashara kirahisi.
Na kama mlivyonieleza kwenye risala yenu wasindakaji wadogo mnaweza kupima
bidhaa zenu na kupata nembo ya T.B.S. Bure.
Juhudi zote hizi ni kuhakikisha wazalishaji wadogo wanaimarika na kupiga
hatua. Tanzania haina makampuni mengi makubwa ya usindikaji wa vyakula,
hivyo mkombozi wa mazao ya shambani, hasa yale yanayoharibika kwa urahisi,
kwa sasa ni huyu mjasiriamali mdogo. Na Serikali inatambua hilo.
Mwenyekiti,
Mimi ni mwenyekiti wa taaasisi isiyo ya kiserikali inayoitwa Wanawake na
Maendeleo. Kazi yake kuu ni kuhamasisha na kusukuma mbele maendeleo ya
wanawake. Nimejaribu kueleza juhudi za serikali kuendeleza wajasiriamali.
Lakini pia napenda niwakumbushe kuwa serikali yetu pia inatoa msukumo na
uwezeshwaji wa makusudi kwa akina mama ili kuhakikisha hawaachwi nyuma
kimaendeleo.
Nimalizie kwa kuwashukuru tena wafadhili wa maonyesho haya. Na sasa natamka
rasmi kuwa maonyesho ya TANOFA ya usindikaji vyakula sasa yamezinduliwa
rasmi.
Ahsanteni sana kwa kunisikiliza